Sunday 30 September 2012

TAMKO LA CHAMA KUKANUSHA SHUTUMA ZA CHAMA CHA CUF KUFANYIWA VURUGU NA CHADEMA.

TAMKO LA CHAMA KUKANUSHA SHUTUMA ZA CHAMA CHA CUF KUFANYIWA VURUGU NA CHADEMA.
Ndugu wananchi na wanahabari,

Siku ya terehe 27 Alhamisi Septemba 2012 chama cha wananchi CUF walitoa taarifa ya malalamiko kwa vyombo vya habari na mitandao kuwa wanachama wa CHADEMA wamewafanyia vurugu kwa kuwapiga mawe na kuwa jambo hilo limehamasishwa na viongozi wa chama katika mkoa wa Arusha pamoja na Mhe Godbless Lema.
Wote tunafahamu kuwa siku hiyo hiyo katika viwanja vya soko la Kilombero wafanyabiashara ndogo ndogo walikuwa wamevamia na walikuwa wakijigawia maeneo, baada ya eneo la awali walilopewa la viwanja vya NMC kushindwa kuwachukua wafanyabiashara wote na halmashauri kushindwa kutoa majibu kwa wafanyabiashara hawa ambao waliwaambia wote waende NMC.
Kwanza tunapenda kutoa pole kwa viongozi wa CUF kwa jambo hili lililowapata. Wao kama watu na Watanzania wenzetu tunawapa pole sana.
Pili, CHADEMA inakanusha kuhusika na jambo hili. Hii si tabia ya CHADEMA na kamwe haiwezi kuwa tabia ya CHADEMA kufanya siasa chafu za namna hiyo. CHADEMA tunajali sana amani na upendo, na hii ndiyo tabia na makuzi yetu Watanzania.
Katika mazingira haya, CHADEMA tunachukua fursa hii kuvikaribisha vyama vyote mathalani CUF, Arusha ni yetu sote na tutumie demokrasia vizuri kufanya kazi nzuri ya siasa kwa ajili ya kusababisha na kuleta matumaini kwa Watanzania hawa ambao serikali ya chama cha mapinduzi imeshindwa kuwaletea.
CHADEMA hatuna shida na ushindani wa kisiasa katika mazingira ya kidemokrasia kwa maana ndio wakati pia wa wananchi kupima na kujua nani mkweli na ama nani anafanya kwa dhati ya kweli. Hivyo tunawakaribisha CUF karibuni Arusha na wala wasitafute kisingizio cha kuegemea ili CUF ianze kutajwa tajwa kwa kutumia mgongo wetu.
Sambamba na hili, CHADEMA mkoa wa Arusha tumesikitishwa sana na tamko la CUF lilitolewa na Naibu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na haki za BInadamu Mhe Abdul Kambaya, tamko lenye matisho na lugha isiyofaa. Moja na maneno ya tamko hilo wamesema, nukuu “Uwezo wa kuwafanya tutakavyo tunao na kwa sababu wameanza tunaweza kumaliza”. Wakazi wa Arusha na Watanzania wapime na waone, haya si maneno yanayoweza kutoka kwenye kichwa cha mtu anayefikiri vizuri, mtu anayeipenda nchi yake na kuheshimu utawala wa sheria. Zaidi ya hapo tamko hilo limesema pia, “Ile ngangari kwa polisi tunaweza kuwahamishia wao wakose pa kukaa”.
Katika yote haya, niwaombe wakazi wa Arusha, Wanachadema na hata wanachama wa vyama vingine tuwapende na tuwakaribishe CUF Arusha na sote tufanye kazi ya siasa kwa nguvu za hoja. CUF wanaweza kufanya hicho wanachotaka kufanya lakini CHADEMA kamwe hatupo tayari kwa vurugu ya aina yoyote, aidha tunawakaribisha kwa moyo mmoja na kama wapo tayari basi tufanye siasa zenye tija na manufaa kwa wakazi wa Arusha.
Aidha nitoe onyo kali sana kwa mamluki ambao wamekuwa wakijifanya kondoo kumbe ndani ni mbwa mwitu. Mara kadhaa watu hawa wamekuwa wakisababisha fujo ili kukifanya CHADEMA kionekane kuwa ni chama cha vurugu. MAMLUKI ni sumu, tukimgundua na kumthibitisha mtu wa aina hiyo katikati yetu tutamtangaza mbele ya jamii kuwa yeye ni sumu na kuomba wananchi wamtenge maana anapingana kwa kuleta hila na unafiki kwenye kazi ya kuwakomboa Watanzania. Niwatangazie mamluki hamtatuweza na tutawagundua tu.
Mwisho, tunapoelekea kwenye marudio ya uchaguzi mdogo kwenye kata za Daraja II kwa Arusha mjini na Bangata kwa wilaya ya Arumeru Magharibi, nirudie kusema maneno ya Mhe Lema kuwa iwapo viongozi na watumishi wa umma watajihusisha na kushiriki kwa kufanya kampeni za kisiasa wakiwa wanatumia magari na vifaa vingine vya serikali watu hawa tutawakamata na tutawapeleka huko wanakostahili kupelekwa wezi na vibaka wengine. Hii ni tahadhari tunamaanisha kweli na wananchi wote wawe makini “wakamate mwizi” lengo likiwa ni kuweka adabu kwa watumishi na viongozi umma wanaovunja sheria ya utumishi wao kwa umma na matumizi ya rasilimali kwa namna isivyotakiwa kisheria. CHADEMA tutashiriki chaguzi hizi na tunawaomba wakazi wote wa maeneo haya tushiriki kwa utulivu na amani.
WANACHADEMA wote tuendelee kuwa majasiri, tusiwe waoga na tusimamie kweli na haki.
“Hakuna kulala Mpaka Kieleweke”
Amani Sam Golugwa
KATIBU WA CHADEMA MKOA WA ARUSHA: golugwa@gmail.com

No comments:

Post a Comment

Chadema UK Ndani ya Milton Keynes

DAR NI SISI - VIDEO MAISHA YA WANADAR HATA BAADA YA MIAKA50 YA UHURU